DAR ES SALAAM
Na Mwandishi Wetu
MWENYEKITI wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Taifa, Mary Chatanda ametoa pongezi kwa uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Temeke (TRRH) kwa juhudi zao za kusimamia na kuboresha huduma za afya. Chitanda amefanya ziara katika hospitali hiyo na kufurahishwa na maendeleo na ubora wa kazi inayofanywa na wataalamu na uongozi wa hospitali hiyo.
Chitanda amesema Hospitali hiyo inafanyakazi kwa uaminifu na kwa uangalifu mkubwa katika kutoa huduma ikiwemo na kusimamia na kuboresha majengo ya hospitali.
Ziara hiyo ilihusisha pia Naibu Mwenyekiti wa UWT, Mhe. Zainab Shomari, pamoja na Katibu Mkuu wa UWT, Mhe. Jokate Mwegelo, na viongozi wengine wa UWT.
Viongozi hao walipata fursa ya kutembelea wodi za kina mama waliojifungua na wale wanaosubiri kujifungua, ambapo walishuhudia juhudi za hospitali katika kutoa huduma bora za afya kwa wananchi.
Kwa upande wake, Mganga Mfawidhi wa Hospitali hiyo, Dkt. Joseph Kimaro, ameeleza mikakati mbalimbali inayofanywa na hospitali kuboresha huduma za afya.
Amesisitiza kuwa hospitali inaendelea kukua na kueleza kuhusu ongezeko la idadi ya madaktari bingwa.
Pia ametangaza mipango ya kuanzisha miradi kama vile usafishaji damu (Dialysis), ambao unatarajiwa kukamilika kwa ushirikiano na mdau wao muhimu, TPA.


0 Maoni