MITIHANI KIDATO CHA NNE KUANZA KESHO

 


Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA), Dk Said Mohamed alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini.

DAR ES SALAAM

Na Mwandishi Wetu

JUMLA ya watahiniwa 572,338 wanatarajiwa kuanza kufanya mtihani wa Taifa wa kidato cha nne kuanzia kesho Novemba 13 hadi Novemba 30, 2023 ambapo kati yao 543,386 ni wa mashule na watahiniwa wa kujitegemea ni 28,952.

 Hayo yamesemwa leo jijini Dar es Salaam na Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA), Dk Said Mohamed alikuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini.

Dkt. Mohamed amesema katika watahaniwa wa shule 543,386 waliosajiliwa wavulana ni 250,237 sawa na asilimia 46.05 na wasichana ni 293,149 sawa na asilimia 53.95.

“Aidha watainiwa wa shule wenye mahitaji maalum ni 614 ambapo kati yao 283 ni wenye uoni hafifu, 24 ni wasioona, 135 wenye ulemavu wa kusikia, 11 ni wenye ulemavu wa akili na 161 ni wenye ulemavu wa viungo vya mwili,”amesema Katibu huyo.

Hata hivyo, ameeleza kuwa kwa mwaka 2022 jumla ya watahiniwa wa shule waliosajiliwa walikuwa 534,753 hivyo kuna ongezeko la jumla ya watahiniwa 8633 sawa na asilimia 1.61 kwa mwaka 2023 ukilinganisha na mwaka 2022.

Watahiniwa wa kujitegemea 28,952 walisajiliwa kati yao wavulana ni 11,867 sawa na asilimia 40.99 na wasichana ni 17,085 sawa na asilimia 59.01.

Amebainisha kati yao wenye mahitaji maalum kwa wanaafunzi wa kujitegemea wakiwa nane kati yao wenye uoni hafifu ni wanne na wasioona wanne.

Akielezea kuhusu maandalizi ya mtihani, Dk Mohamed amesema yamekamilika ikiwa ni pamoja na kusambazwa kwa mitihani ,vijitabu vya kujibia na nyaraka zote muhimu zinazohusu mitihani husika katika mikoa yote Tanzania Bara na Zanzibar.

Aidha Katibu huyo ametoa wito kwa kamati za mitihani za mikoa na Halmashauri kuhakikisha usalama wa vituo vya mitihani unaimarishwa na vinatumika kwa mujibu wa mwongozo uliotolewa na Baraza.

“Kwa  upande wa  wasimammizi walioteuliwa  kusimamia  mtihani wahakikishe wanafanya kazi yao ya usimamizi kwa umakini na uadilifu wa hali ya juu,”amesema.

Kwa upande wa watahiniwa, Baraza hilo limewataka kufanya mitihani kwa kuzingatia kanuni za mitihani na kueleza kuwa halitarajii kuona mtahiniwa yoyote kujihusisha na vitendo vya udanganyifu.

“Mtahiniwa yoyote atakayebainika kufanya udanganyifu, matokeo yake yatafutwa kwa mujibu wa kanuni za mtihani,”amesisitiza Katibu huyo.

Kwa upande wa wamiliki wa shule na wakuu wa shule, Dk Mohamed amesema kwa namna yoyote hawatakiwi kuingilia majukumu ya wasimamizi wa mtihani katika kipindi chote cha ufanyikaji mtihani huo.

Amesema baraza halitasita kukifuta kituo chochote cha mtihani endapo litajiridhisha pasipo shaka kuwa uwepo wake unahatarisha usalama wa mtihani.

“Aidha wakuu wa shule wahakikishe wanatekeleza majukumu yao ya usimamizi kwa kuzingatia mwongozo wa usimamizi ukiotolewa na Baraza na kuepeuka kuingilia usimamizi wa watahiniwa ndani ya vyumba vya mitihani,”amesema.

Pia baraza hilo limetoa wito kwa jamii  kutoa ushirikiano unaotakiwa kuhakikisha mtihani wa kidato cha nne na maarifa 2023 unafanyika kwa amani na utulivu.

“Wananchi wanaombwa kuhakikisha kuwa hakuna mtu yoyote asiyehusika na mtihani anaingia kwenye maeneo ya shule katika kipindi chote cha mtihani kwani kwa kufanya hivyo tunawezesha wanafunzi kufanya mtihanni kwa amani na utulivu,”amesema

 

 

Chapisha Maoni

0 Maoni