Dar es Salaam;
Mamlaka
ya hali ya hewa nchini TMA imesema inatambua mchango mkubwa wa vyombo
vya habari katika kutoa taarifa sahihi na kwa wakati juu ya hali ya hewa
kwa wananchi.
Hayo yalisemwa na mgeni rasmi,
Mwenyekiti wa Bodi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dkt.
Buruhani Nyenzi wakati wa hafla ya utoaji tuzo ya mwanahabari bora wa
habari za hali ya hewa kwa mwaka 2023, iliyofanyika katika ukumbi wa
mikutano wa Chuo cha Biashara (CBE), Dar es Salaam, Tarehe 30 Oktoba
2023.
"Ni furaha kubwa kuungana nanyi katika
utoaji wa Tuzo mbalimbali ambazo ni ishara ya kutambua na kuthamini
mchango na mafanikio yenu katika utoaji wa habari na taarifa za hali ya
hewa kwa Jamii”. Alisema Dkt. Nyenzi.
Alisema
kwa kutambua mchango wao mamlaka hiyo imekuwa ikitoa tuzo kwa waandishi
wa habari kila mwaka ambao wamekuwa wakitangaza na kuchaputa taarifa za
hali ya hewa nchini kwa lengo la kuongeza hamasa na kutambua mchango
wao.
Alitangaza majina ya washindi wa tuzo za
mwaka huu ambapo mshindi wa tuzo ya jumla ni Bw. Mussa Kharid kutoka
Kiss FM, mshindi wa upande wa magazeti alikuwa Bi. Pamela Chilongola
kutoka gazeti la Mwananchi na mshindi wa upande wa mitandao ya kijamii
alikuwa Noel Rukanuga kutoka Uhondo TV.
Kwa
upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la
Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC)
Dkt. Ladislaus Chang’a aliwaeleza wanahabari kuwa Mamlaka itaendelea
kuboresha na kupanua wigo wa Tuzo za Wanahabari Bora wa taarifa za hali
ya hewa na mabadiliko ya tabianchi kadri inavyowezekana, na aliwaomba
wanahabari watoe maoni na mapendekezo ya namna bora ya kupanua wigo wa
utoaji Tuzo ili kuendelea kuchagiza mwamko na umahili katika kutoa elimu
na kusambaza tarifa za hali ya hewa.
0 Maoni